![]() |
Samatta kushoto katika moja ya mechi za Mazembe zilizopita |
Na Prince Akbar
TOUT
Puissant Mazembe imelazimishwa sare ya bila kufungana na mabingwa wa Afrika,
Esperance ya Tunisia katika Nusu Fainali ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika jioni
ya leo kwenye Uwanja wa Stade du TP Mazembe mjini Lubumbashi, Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Katika mchezo
huo, Mazembe ilipata pigo kutokana na beki wake tegemeo, Stopila Sunzu kutolewa
nje kwa kadi ya pili ya njano (nyekundu) dakika ya pili ya muda wa nyongeza baada
ya kutimu dakika 90 za kawaida.
Awali, Sunzu
kaka wa mshambuliaji wa Simba, Felix Sunzu, alionyeshwa kadi ya kwanza ya njano
dakika ya kwanza ya muda wa nyongeza baada ya kutimu dakika 45 za kipindi cha
kwanza.
Washambuliaji
wote wawili wa Kitanzania walicheza mechi hiyo, Mbwana Ally Samatta alicheza
hadi dakika 83 alipompisha Sinkala, wakati Thomas Emanuel Ulimwengu alitokea
benchi dakika ya 58 kwenda kuchukua nafasi ya D. Kanda.
Matokeo haya
yanamaanisha Nusu Fainali ya pili mjini Tunis itakuwa kali zaidi na hata sare
yoyote ya mabao itaipeleka Mazembe fainali.
Katika Nusu
Fainali nyingine ya kwanza iliyochezwa jana, mabingwa mara sita Afrika, Al Ahly
ya Misri walilazimisha sare ya kufungana mabao 3-3 na Sunshine Stars ya Nigeria
katika mechi ya kwanza ya Nusu Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika jana
iliyopigwa huko Ijebu-Ode kwenye Uwanja wa kimataifa wa Dipo Dina.
Nahodha wa Sunshine,
Godfrey Oboabona aliikosa mechi hiyo baada ya kuonyeshwa kadi ya pili ya njano
katika mechi ya mwisho ya makundi dhidi ya Esperance ya Tunisia, wakati Mohamed
Aboutrika anatumikia adhabu ya kufungiwa miezi miwili na Ahly.
Ahly ilipata
bao la kwanza dakika ya 18 kupitia kwa Mohamed Nagy, aliyefumua shuti kutoka
nje ya boksi na kumtungua Moses Ocheje, kabla ya Mahdy El Sayed kuifungia bao
la pili timu hiyo dakika ya 30, wakati Sunshine ilipata bao la kwanza dakika ya
40, kupitia kwa kiungo Mcameroon, Tamen Medrano aliyemtungua kwa shuti la mbali
kipa wa Ahly, Sherif Elkramy.
Wenyeji
walisawazisha dakika ya 73 kwa mkwaju wa penalti wa Dele Olorundare baada ya Ajani
Ibrahim kuangushwa kwenye eneo la hatari na Mohamed Nagy.
Pamoja na
hayo, Mashetani Wekundu wa Cairo walipata bao lililoelekea kuwa la ushindi, dakika
moja badaaye kupitia kwa kijana mwenye umri wa miaka 25, Nagy ambalo lilikuwa
bao lake la pili kwenye mechi hiyo.
Beki wa Sunshine,
Precious Osasco aliisawazishia timu yake dakika ya 83 kwa shuti la mpira wa
adhabu lililomshinda kipa Elkramy. Nagy alipata
nafasi ya kukamilisha hat-trick dakika tatu kabla ya filimbi ya mwisho, lakini
kichwa chake kiliupaisha mpira alipokuwa anaunganisha kona. Mechi za marudiano zitachezwa
wiki ijayo.