![]() |
Simba SC |
Na Mahmoud Zubeiry
LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara,
inatarajiwa kuendelea leo kwa timu 10 kupambana kwenye viwanja vitano tofauti
katika raundi ya saba ya ligi hiyo yenye timu 14, macho na masikio ya wengi
yakielekezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga ambako mabingwa watetezi, Simba
SC watakuwa wakimenyana na mabingwa wa 1988, Coastal Union.
Vigogo wa Friends Of Simba (F.O.S)
wakiongozwa na Mwenyekiti wao, Zacharia Hans Poppe wamekodi ndege kwenda Tanga
kuwaongezea morali washinde mechi ya leo, ambayo inatarajiwa kuwa ngumu
kutokana wenyeji kupania kuwa timu ya kwanza kuifunga Simba msimu huu.
Ikumbukwe Simba imetoa sare moja ya
kufungana 1-1 na Yanga, Oktoba 3, mwaka huu katika mechi zake sita ilizocheza
sasa na nyingine zote tano imeshinda, jambo ambalo linawafanya waendelee kuwa
kileleni mwa Ligi Kuu.
Simba, ambayo kwenye mechi hiyo
itawakosa nyota wake saba, Emanuel Okwi ambaye amekwenda kujiunga na timu yake
ya taifa, Uganda, Ramadhani Chombo ‘Redondo’, Mrisho Khalfan Ngassa
wanaosumbuliwa na Malaria, Haruna Shamte, Kiggi Makassy Kiggi, Hamadi Waziri na
Komabil Keita ambao ni majeruhi ipo Tanga tangu Jumatano.
Wachezaji 22 walio na timu Tanga ni
makipa Juma Kaseja, Wilbert Mweta, mabeki Nassor Masoud ‘Chollo’, Amir Maftah, Juma
Nyoso, Paschal Ochieng, Shomary Kapombe, Hassan Khatib, Paulo Ngalema, Komabil
Keita, viungo Mwinyi Kazimoto, Jonas Mkude, Amri Kiemba, Salim Kinje, Ramadhani
Singano, Uhuru Suleiman, Haruna Moshi ‘Boban’ na washambuliaji Felix Sunzu,
Edward Christopher, Haroun Chanongo, Daniel Akuffo na Abdallah Juma.
Katika kujiandaa na mechi ya leo,
ambayo itachezeshwa na refa Simon Mberwa kutoka Pwani akisaidiwa na Godfrey
Kihwili na Abdallah Uhako wote kutoka Arusha, Simba Jumanne ilicheza mechi ya
kujipima nguvu na kuifunga Azam FC mabao 3-2 katika mchezo wa kirafiki
uliofanyika asubuhi kwenye Uwanja wa Chamazi, maarufu kama Azam Complex, nje
kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.
Mabao ya Simba siku hiyo yalifungwa
Ramadhani Singano ‘Messi’, Uhuru Suleiman ‘Robinho’ na Daniel Akuffo, wakati ya
Azam yalifungwa na Jamil Mchauru na Khamis Mcha.
Hiyo ilikuwa mechi ya nne Azam
inafungwa na Simba msimu huu katika mechi tano walizokutana hadi sasa, baada ya
awali kufungwa kwa penalti kwenye fainali ya Kombe la Urafiki, kufuatia sare ya
2-2, kufungwa 2-1 kwenye Nusu Fainali ya BancABC Sup8R na 3-2 kwenye mechi ya
Ngao ya Jamii, wakati wao walishinda 3-1 dhidi ya Wekundu hao wa Msimbazi,
katika Robo Fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame.
Azam na Simba zitakutana tena
katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, mzunguko wa kwanza, Oktoba
27, mwaka huu, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Simba ndio inaongoza Ligi Kuu, hadi
sasa ikiwa imeshinda mechi tano kati ya sita ilizocheza na moja tu imetoka
sare, hivyo kujikusanyia pointi 16, wakati Azam inashika nafasi ya pili
ikizidiwa pointi tatu, ingawa pia iko nyuma kwa mchezo mmoja.
Katika mechi ya leo, Simba SC
inawahofia zaidi wachezaji wake wa zamani ambao kwa sasa wanachezea Coastal.
Gumzo ndani ya Simba kuelekea
mchezo huo ni namna ambavyo wachezaji wao waliowatema na sasa wanachezea
Coastal watakavyojituma katika mechi hiyo ili kuonyesha wao bado wachezaji
wazuri.
Wachezaji wa zamani wa Simba kwenye
kikosi cha Cosatal ni mabeki Said Swedi ambaye ni Nahodha wa timu, Juma Jabu,
kiungo Jerry Santo na washambuliaji Nsa Job na Sali Aziz Gilla.
Wachezaji wote hao huwa wanaanza
kwenye kikosi cha kwanza cha Cosatal na leo pia, kuna uwezekano Swedi
‘Panucci’ akaanza beki ya kulia na JJ akacheza kushoto, wakati kwenye kiungo
Mkenya, Santo ataichezesha timu.
Kuna uwezekano mkubwa sana Salim
Aziz Gilla akatokea benchi, lakini ‘piga ua’, mkali wa mabao, Nsa Job lazima
ataanza kwenye mechi hiyo kujaribu kufanya kile alichokifanya msimu uliopita
akiwa Villa Squad, kutikisa nyavu za Simba kwa bao muhimu.
Lakini pia, kikosi cha mabingwa hao
wa Ligi Kuu 1988, kina wachezaji wengine wa kutisha kama kiungo Razack Khalfan
aliyewahi kucheza Yanga na mshambuliaji wa timu ya taifa ya vijana chini ya
umri wa miaka 20, Atupele Green, ambaye huenda akaanza na Nsa leo pale mbele.
Katika mechi nyingine, Polisi
Morogoro itaikaribisha Azam kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro wakati refa
wa FIFA, Oden Mbaga atakuwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya
kuchezesha mechi kati ya wenyeji Tanzania Prisons na Oljoro JKT.
Mechi nyingine za leo ni Ruvu
Shooting dhidi ya African Lyon kwenye Uwanja wa Mabatini, Mlandizi, na Mtibwa
Sugar watacheza na Mgambo Shooting kwenye Uwanja wa Manungu, Turiani mkoani
Morogoro.