Ochieng katika mechi ya juzi |
Na Mahmoud Zubeiry
KOCHA wa
Simba SC, Mserbia Profesa Milovan Cirkovick amesema kwamba amevutiwa na uwezo
wa beki Mkenya, Paschal Ochieng katika mechi ya juzi dhidi ya Coastal Union
kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
Akizungumza
na BIN
ZUBEIRY baada ya mechi hiyo iliyoisha kwa sare ya bila kufungana,
Milovan alisema kwamba amevutiwa mno na uwezo wa Ochieng na kwamba sasa anaweza
kuendelea kupata nafasi kwenye kikosi cha kwanza.
Lakini Milovan
alisema hakuvutiwa kabisa na uchezaji wa mshambuliaji Daniel Akuffo kutoka
Ghana.
“Sikuvutiwa
kabisa na Akuffo,”alisema Cirkovick ambaye pia alisikitika kuwakosa wachezaji
wake watatu nyota, Mrisho Ngassa, Ramadhan Chombo ‘Redondo’ ambao ni wagonjwa
na Okwi, aliyekwenda kuichezea timu ya taifa ya Uganda, dhidi ya Zambia kuwania
tiketi ya kucheza Fainali za Mataifa ya Afrika mwakani.
Simba
iliorejea Dar es Salaam jana na leo inatarajiwa kuendelea na mazoezi kwenye
Uwanja wa Kinesi, kujiandaa na mchezo ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania
Bara, dhidi ya Kagera Sugar Jumatano Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Katika
mchezo huo, Simba inatarajiwa kuwapokea wachezaji wake watatu iliyowakosa
kwenye mechi ya juzi, Okwi, Ngassa na Redondo.
Okwi
anatarajiwa kurejea Dar es Salaam leo, wakati Ngassa na Redondo tayari wamepona
na leo wanaanza mazoezi na timu hiyo.
Mechi
nyingine za Jumatano zitakuwa kati ya Prisons na Azam FC kwenye Uwanja wa
Sokoine, Mbeya, Polisi Morogoro na JKT Ruvu Uwanja wa Jamhuri, Morogoro, Mgambo
JKT na Toto Africans Uwanja wa Mkwakwani, Tanga na JKT Oljoro dhidi ya African
Lyon Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha.
Simba bado
ipo kileleni mwa Ligi Kuu kwa pointi zake 17, baada ya kucheza mechi saba,
ikifuatiwa na Azam FC yenye pointi 16, ambayo hata hivyo imecheza mechi sita,
wakati Yanga inashika nafasi ya tatu kwa pointi zake 11, baada ya kucheza mechi
saba pia.