Said Bahanuzi |
Na Mahmoud Zubeiry
KLABU ya
Yanga ya Dar es Salaam, inatarajiwa kuingia kambini leo kujiandaa na mchezo wao
ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Ruvu Shooting Jumamosi wiki
hii kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Yanga ambayo
katika mechi yake ya mwisho iliifunga Toto Africa mabao 3-1 mjini Mwanza,
itaweka kambi kwenye hoteli ya Uplands, Changanyikeni, Dar es Salaam uku
ikifanya mazoezi kwenye Uwanja wa sekondari ya Loyola, Mabibo, Jijini.
Yanga
itaendelea kuwakosa mazoezini wachezaji wake wawili majeruhi, beki Kevin Yondan
na mshambuliaji Said Bahanuzi.
Bahanuzi
‘Spider Man’ anatarajiwa kuanza mazoezi mepesi leo kufuatia kuchanika nyama za
paja la mguu wa kulia katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi
ya Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba Jumatatu wiki iliyopita.
Bahanuzi
aliumia dakika ya 23, baada ya kugongana na beki Benjamin Effe wa Kagera Sugar
na kushindwa kuendelea na mchezo, nafasi yake ikichukuliwa na Jerry Tegete
katika mechi ambayo Yanga ililala 1-0, beo pekee la Themi Felix.
Daktari wa
Yanga, Sufiani Juma aliiambia BIN ZUBEIRY mwishoni mwa wiki
kwamba, mfungaji huyo bora wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la
Kagame, anaendelea vizuri baada ya kuchanika nyama za paja la mguu wa kulia.
“Lini haswa
ataingia kwenye programu kamili ya mazoezi, itategemea na maendeleo yake
atakapoanza mazoezi mepesi,”alisema Sufiani.
Kuhusu beki
Kevin Yondan aliyeumia kwenye mechi dhidi ya Simba SC, Oktoba 3, mwaka huu
baada ya kugongwa na Haruna Moshi ‘Boban’, Sufiani alisema naye anaendelea
vizuri na wakati wowote wiki hii ataanza mazoezi mepesi.
Zaidi ya
hao, Sufiani alisema Yanga ina majeruhi mwingine mmoja tu, ambaye ni Salum
Telela ambaye naye anaendelea vizuri.
Bahanuzi
ndiye tegemeo la mabao la Yanga kwa sasa, kwani tangu ajiunge na timu hiyo
akitokea Mtibwa Sugar msimu huu, ameifungia mabao 12 katika mechi 13, ikiwemo
ile dhidi ya Kagera aliyocheza kwa dakika 23 kabla ya kuumia na kutoka.
Yanga kwa
sasa inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu kwa pointi zake 11,
baada ya kucheza saba, kushinda tatu, sare mbili na kufungwa mbili.
Simba
iliyocheza mechi saba pia, inaongoza ligi hiyo kwa pointi zake 17, ikifuatiwa
na Azam FC yenye pointi 16, iliyocheza mechi sita.