• HABARI MPYA

    Sunday, May 20, 2012

    TUMLILIE MAFISANGO HUKU TUKIJIFUNZA


    Mafisango katika picha tofauti

    MWILI wa kiungo wa kimataifa wa Rwanda, Patrick Mutesa Mafisango ulitarajiwa kuzikwa leo nyumbani kwao mjini Kinshasa, Jamhuri ya Kidemokrsaia ya Kongo (DRC).
    Mafisango alifariki dunia kwa ajali ya gari, usiku wa kuamkia Alhamisi, maeneo ya VETA, Dar es Salaam, akiwa anatoka disko, Club Maisha na gari lake kuacha njia na kutumbukia mtaroni wakati akimkwepa dereva wa pikipiki.
    Kifo chake kimeacha pengo katika klabu yake, Simba SC na timu yake ya taifa, Amavubi Stars. Hakuna anayekufa kwa taarifa, lakini kwa kuwa Mafisango hakuugua bali ajali tu imechukua uhai wake, kifo chake ni aina ya vifo vinavyoitwa vya ghafla.
    Amefariki katika wakati ambao, klabu yake ilikuwa inatarajia mengi kutoka kwake. Huyu alikuwa mchezaji tegemeo kwenye kikosi cha Simba na hakuna kingine kilichokuwa kinamfanya awe tegemeo zaidi ya jitihada zake uwanjani.
    Makala nyingi ziliandikwa kwa ajili yake mwezi uliopita wakati aliposimamishwa na uongozi wa klabu yake kwa utovu wa nidhamu, kabla ya kusamehewa siku moja baadaye kabla ya timu kwenda kurudiana na ES Setif ya Algeria katika Kombe la Shirikisho.
    Wachambuzi wa nyumbani waliandika wakisema, kweli nje ya Uwanja Mafisango anaweza kuwa mtovu wa nidhamu, lakini uwanjani ni ‘habari nyingine’. Walimsifu kwa soka yake na kuusihi uongozi wa Simba kutafuta namna ya kuendelea kuishi na mchezaji huyo.
    Huyu ni mchezaji ambaye amefunga mabao 11 katika Ligi Kuu msimu huu, pamoja na kwamba katika kipindi hicho alisimamishwa mara mbili kwenye klabu hiyo na kukosa mechi zisizopungua tano.
    Huyu ni mchezaji wa nafasi ya kiungo, ambaye tena mara nyingi hucheza kama kiungo mkabaji. Huyu ni mchezaji ambaye alikuja nchini kama beki wa kushoto akisajiliwa na Azam FC mwaka juzi.
    Azam FC ilimuacha aende Simba, baada ya kushindwa kuvumilia utovu wake wa nidhamu. Na ni utovu upi wa nidhamu alikuwa nao Mafisango? Pombe. Jamaa alikuwa anapenda pombe na kujirusha hivyo wakati mwingine kuingilia programu za mazoezi za makocha.
    Alikuwa anaweza akaenda kustarehe, kesho yake akachelewa kuamka na kuchelewa mazoezini, jambo ambalo lilikuwa linawakera makocha kuanzia Mganda Moses Basena aliyempokea Simba hadi sasa Mserbia, Milovan Cirkovick.
    Lakini akishaomba radhi, Mafisango alikuwa mtu safi sana. Alikuwa anaweza kumfanya mwalimu asahau yote anapokuwa uwanjani. Rage alisema huyo alikuwa mchezaji wa kipekee, hakukosea- kwa kumlinganisha na wachezaji wengi wa Tanzania, Patrick alikuwa wa kipekee mno.
    Alikuwa anajituma mno uwanjani. Alikuwa mchezaji wa timu kwa ajili ya ushindi. Anapopanda kutoka kwenye dimba dogo kwenda kwenye D ya wapinzani kusaidia mashambulizi, akipoteza au mpira ukipotea alikuwa akirudi kwa kasi na kwa mipango kuziba nafasi yake.
    Alikuwa ana akili sana ya mpira. Hakuwa fundi sana, ila alikuwa ana jitihada mno uwanjani.
    Anapofanya kosa, ambalo kwa namna moja au nyingine anaweza kuhisi amewaudhi mashabiki, Patrick alikuwa anahakikisha kabla ya kipyenga cha mwisho mashabiki wamefurahi kwa ajili yake.
    Mfano ni katika mechi ya kwanza na Al Ahly Shandy mjini Dar es Salaam, Mafisango baada ya kukosa penalti, alipigana hadi akafunga. Alikuwa hata akipoteza pasi, anahakikisha mpira unarudi tena kwenye himaya yao.
    Alikuwa ni mchezaji ambaye kocha yeyote angependa kuwa naye kwenye timu yake. Simba imepoteza mchezaji mmoja siyo tu mzuri, bali muhimu kwenye kikosi chake. Felix Sunzu anaweza pia kuzungumza Kifaransa na Kilingala- lakini bado Mafisango alikuwa ana faida za ziada ndani ya Simba SC.
    Kila unapolitazama Kombe la ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu- kwa mabao yake 11, wazi Mafisango ana mchango mkubwa. Japokuwa, baada ya kifo chake, Simba ilimtoa mchezaji wake Haruna Moshi ‘Boban’ na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Kinesi wasindikize mwili wake DRC- lakini kwa soka yake kama ingekuwa kusajiliwa ungekwenda Ujumbe mzito zaidi wa Simba kumfuata Kinshasa.
    Basi tena, mwandamu ukishafumba macho watu wanasahau yote. Ilinipa tabu kidogo kuelekewa, Mwenyekiei wa Simba Alhaj Ismail Aden Rage, Makamu wake Geoffrey Nyange ‘Kaburu kwa nini mmoja wao asiende na mwili wa marehemu DRC?
    Ila, Rage alisafiri hadi Cerpe Verde kufuata ITC ya Gervais Kago, kwa sababu alikuwa anataka mchezaji- Kaburu amekwishasafiri sana kufuata wachezaji nchi za nje, lakini mwili wa marehemu aliyekuwa mpiganaji na mwenye mchango mkubwa kwenye klabu, ilikuwa rahisi tu kuamua Boban na Kinesi waende.
    Boban amekwenda na angekwenda tu, kwa sababu yule alikuwa rafiki yake mkubwa- ila familia ya marehemu imeupokea mwili wa Mafisango kutoka kwa Kinesi leo, Mjumbe tu wa Kamati ya Utendaji.
    Si mada yangu hiyo leo. Nachotaka kuwaambia wachezaji wa Tanzania, wamejifunza nini kutokana na Mafisango katika kipindi chake cha miaka miwili ya kufanya kazi Tanzania?
    Rais Jakaya Kikwete alisema wakati akitoa salamu zake za rambirambi kwa Simba, kwamba mchezaji huyo amechangia maendeleo ya soka ya Tanzania kwa kipindi kifupi cha kucheza nchini.
    Hapewi sifa kwa sababu ni kawaida yetu kusifia wafu, lakini takwimu zinasema alikuwa hodari kweli. Pasi ngapi za mabao, mabao mangapi amefunga msimu huu akiwa Simba pamoja na kwamba alisimamishwa mara mbili kwa utovu wa nidhamu?
    Wale waliopata fursa ya kucheza msimu mzima watazame wamezifanyia nini klabu zao? Lakini walikuwa wanamuona Mafisango uwanjani anavyocheza, anavyojituma uwanjani- hili ni somo gani kwao?
    Juma Seif ‘Kijiko’, alikuwa kiungo wa ulinzi wa Yanga siku Mafisango akiiongoza Simba kushinda 2-0 na kuteuliwa mchezaji bora wa mechi ya Ngao ya Jamii Agosti mwaka jana- amejifunza nini?
    Si Kijiko tu, hata wachezaji wa Simba, akiwemo Boban mwenyewe ambaye mara nyingi anapopoteza mipira hutembea, wamejifiunza nini kwa Mafisango? Tumlilie Mafisango huku pia tukijifunza kutoka kwake. Hii ni kwa wachezaji wote nchi nzima.
    Kama ana dhambi, namuombea ahueni mbele ya Mwenyezi Mungu Mafisango. Amuepushe na adhabu za kaburi na ampumzishe kwa amani. Amin.   
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TUMLILIE MAFISANGO HUKU TUKIJIFUNZA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top