• HABARI MPYA

    Wednesday, June 06, 2012

    SAMATTA HAPO TU DRC, NIZAR ALIKUWA ANAKIPIGA MAREKANI!

    TIMU ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, ilipigana kiume katika mchezo wa kwanza wa Kundi C ugenini wa kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la Dunia mwaka 2014 dhidi ya wenyeji Ivory Coast, ikifungwa mabao 2-0 kwa taabu.
    Nasema kwa tabu, kwa sababu bao la pili la Ivory Coast lililofungwa na Nahodha wao, Didier Drogba, lilipatikana dakika 10 baada ya beki wa Stars, Aggrey Morris kutolewa nje kwa kadi nyekundu, zikiwa zimebaki dakika 10 kabla ya mchezo kumalizika.
    Lakini pia mechi kama hizi zina mahesabu yake na mavuno zaidi huwa ni kwenye mechi za nyumbani, wakati ugenini matokeo mazuri ni sare au ukimkuta mwenyeji amechoka unamachapa, lakini bado pointi za nyumbani ndio huzibeba timu nyingi kufuzu.
    Kuanza vizuri kwa Stars katika mechi za makundi kuwania kucheza michuano mikubwa ya kimataifa limekuwa jambo la kawaida kwa takriban miaka sita sasa, lakini ajabu mechi zinazofuata Stars hudorora kabla ya kuzinduka mwishoni tena.
    Nitakumbusha; kuelekea fainali za Mataifa ya Afrika Ghana mwaka 2008, Stars ilianza kwa kuifunga Burkina Faso 2-1 katika mchezo wa kwanza- lakini baadaye katika mechi ya tatu ilifungwa na Senegal 4-0, ikalazimishwa sare ya 0-0 nyumbani na Simba hao wa Teranga kabla ya kufungwa mechi ya mwisho na Msumbiji 1-0, ambao mechi ya kwanza ilitoka nao sare ya bila kufungana kwao.
    Tukakosa tiketi ya kwenda Ghana- wakati kuelekea Angola na Afrika Kusini 2010, tuliboronga vibaya, tukilazimishwa sare mbili nyumbani na Mauritius 1-1 na Cameroon 0-0, tukafungwa ugenini na Cameroon 2-1 na Carpe Verde 1-0, wakati ugenini tulishinda mechi moja tu na Mauritius 4-1- na nyumbani tukashinda pia mechi moja na Carpe Verde 3-1.
    Tukakosa tiketi ya kwenda Angola au Afrika Kusini, tukafukuza kocha, Mbtrazil Marcio Maximo na kuajiri Mdenmark, Jan Borge Poulsen. Tukaingia kwenye kinyang’anyiro cha kuwania tiketi ya Gabon na Equatorial Guinea 2012, ambako pia nako tulianza vema kwa sare ya ugenini ya 1-1 na wenyeji Algeria.
    Wengi wakiamini timu imeimarika, mechi ya pili tukafungwa nyumbani 1-0 na Morocco na mechi iliyofuata tukaenda kufungwa tena na Jamhuri ya Afrika ya Kati 2-1 wakati, mechi pekee tuliyofanikiwa kushinda nyumbani ni dhidi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati 2-1, huku mechi mbili nyingine tukifungwa na Morocco 3-1 na moja na Algeria tukitoka sare tena 1-1.  
    Sasa tumeanza na kipigo cha 2-0 ugenini na Jumamosi tuna mechi ya nyumbani dhidi ya Gambia katika Kundi letu. Timu imerejea jana na leo inaanza maaoezi rasmi kwa ajili ya mechi hiyo na Watanzania wana kiu kweli na kucheza fainali za 2014 Brazil, ambazo kama tukifanikiwa zitakuwa za kwanza kwetu.
    Ni vigumu, lakini sioni kwa nini tushindwe ikiwa Angola walicheza fainali za mwaka 2006 Ujerumani. Ni mipango tu ambayo sisi bado hatuna.

    NINI TATIZO LETU?
    Hilo ndilo swali ambalo tunapaswa kujiuliza, soka yetu imekuwa kama homa za vipindi inapanda na kushuka. Haina matokeo ya kufululiza iwe mabaya au mazuri. Tatizo nini, wachezaji, makocha, au uongozi mbovu wa TFF?
    Tumekwishafukuza makocha wawili, Maximo na Poulsen na wachezaji wamebadilishwa sana. Nini bado tatizo?
    Kujitambua na kukosa maono ya mbali kwa wachezaji wetu, ni moja ya matatizo, ambalo leo nitalizungumzia, ingawa yapo mengine kama uongozi mbovu wa TFF yetu ya sasa chini ya Leodegar Chilla Tenga.
    Kwa  nini wachezaji? Beki wa zamani wa Chelsea, Mnigeria Celestine Babayaro alipokuwa Nairobi miezi miwili iliyopita katika ziara ya Kombe la Ligi ya Mabingwa Ulaya, alisema kwamba tatizo la soka ya Afrika ni uongozi mbovu. Kumbe tatizo hili ni la Afrika nzima na si Tanzania pekee, lakini nchi nyingine, wachezaji wake wanapiga hatua na kwa uwezo wao, wanazisaidia hadi timu zao za taifa kupata matokeo mazuri, mfano Zambia mabingwa watetezi wa Afrika.
    Hiyo ni kwa sababu wachezaji wa nchi hizo, kwanza wanakuwa na ndoto binafsi za kutimiza kisoka na wanapigana kutimiza ndoto zao- kubwa kucheza Ulaya kwa ajili ya kunufaika kifedha.
    Katika kuelekea kwenye safari hiyo, wanajikuta wanajituma katika timu zao za taifa, ili kutafuta vigezo vya kucheza Ulaya na hapo ndipo timu zao za taifa zinanufaika nao na wao wananufaika pia kwa kutimiza ndoto zao.
    Lakini kwa wachezaji wetu wa Tanzania, hali ni tofauti sana- mchezaji hujituma mwanzoni tu, ila akishaandikwa na magazeti ya kibongo na kusifiwa kidogo, anavimba kichwa na kiwango kinaanza kushuka hata kabla hakijapanda.
    Sitaki kuuliza nani yuko wapi- ila turejee kikosi kilichocheza na Cameroon katika sare ya 0-0 Dar es Salaam, kati ya 11 walioanza siku hiyo, wangapi wataanza tena Jumamosi na Gambia?
    Wachezaji wetu wanachoka haraka sana. Kwa nini? Ule usemi wa wahenga sifa zinaua, tena zinawaua kweli wachezaji wetu. Wakisifiwa kidogo tu wanavimba vichwa, wanaota ‘majipu’ kwapani, hata salamu inakuwa taabu sana, juhudi mazoezini inashuka na siku mbili tu naye soka inamtoroka mguuni, anabaki mtu wa kelele.
    Nimesikitika sana, Nizar Khalfan anasema amesaini Yanga, akitokea Ligi Kuu ya Marekani na wakati huo huo, leo Danny Mrwanda anaweza kusaini Simba. Wachezaji wetu hawawezi hata kucheza nje!
    Angalau siku hizi wanasema ukweli, zamani walikuwa wana tabia wakienda nje, wakirudi na kukutana na Waandishi wanasema, wamerudi mara moja kwa matatizo ya kifamilia na watarejea muda si mrefu, mwishowe unamsikia amesaini hapa hapa tena.
    Siku hizi wanasema, mkataba wangu umeisha, sijaongezewa, nimerudi nyumbani. Nakumbuka mwaka 1999 katika hafla za tuzo za TASWA, rais Jakaya Kikwete wakati huo akiwa bado Wizara ya Mambo ya Nje, alizungumzia matatizo ya wachezaji wetu kushindwa kucheza nje, na akatoa mfano huo huo wanaporudi, husema wamekuja mara moja.
    Wakati umefika sasa, wachezaji wetu wa kizazi kipya akina Shomary Kapombe, Jonas Mkude na Juma Abdul, wajifunze kutokana na makosa ya kaka zao, ili miaka ijayo tuwe na aina mpya ya wachezaji.
    Wachezaji ambao, kwanza watakuwa ndoto na matarajio na pili kuwa na kiu ya kweli na dhamira ya dhati ya kutimiza ndoto na matarajio yao. Wachezaji ambao watakuwa na maono ya mbali, ambao hawatavimbishwa vichwa na ‘headlines’ za Mwanaspoti, zinazosifia ‘mpaka basi’.
    Lakini, hata kwa wachezaji wa sasa wa timu ya taifa, wanapaswa kujua siri ya kufanya vizuri uwanjani ni kujituma mazoezini na kusikiliza kwa makini mafundisho ya makocha. Ajabu wachezaji wa siku hizi wana dharau, hawajitumi mazoezini, hawasikilizi makocha, halafu wanasema makocha siyo wazuri.
    Unakuta Stars hii iliyopo kambini hivi sasa, kuna wachezaji wanamheshimu kocha Mkuu tu, Mdenmark, Kim Poulsen tu, hawawaheshimu makocha wasaidizi akina Sylvester Marsh na Juma Pondamali wala Meneja wao, Leopold Mukebezi. Namna hii utategemea nini?
    Lazima wachezaji wabadilike na wawe na nidhamu- kwani huo ndio msingi wa mafanikio. Pia, wachezaji wetu kwenye mechi hawana juhudi zozote. Hawajitumi. Hawapigani. Wanacheza utafikiri waliingia kwenye kambi ya timu ya taifa wakitokea Borussia Dortmund, FC Twente, Napoli, Marseille, Spurs au Bilbao, kumbe wametokea kwa Mnyamani wengine kwa Tumbo tu hapo na wana safari ndefu kuelekea kwenye kilele cha mafanikio. Wanaridhika nini? Sijui!
    Bado naamini maisha yako unayakwamisha au kuyafanikisha wewe mwenyewe kulingana na akili, fikra na jitihada zako. Kama wachezaji wetu wanaona kucheza TP Mazembe ni kilele cha mafanikio yao, basi itakuwa hivyo, lakini kama watataka kuvunja rekodi ya Sunday Manara, au Kassim Manara, basi watafanikiwa.
    Nataka nimzungumzie mchezaji mmoja wa Stars hivi sasa, Mbwana Ally Samatta ‘Sama Goal’ kama mfano- kwa sasa anakabiliwa na changamoto kubwa ya kufanya mageuzi kwa wachezaji wa Tanzania- kwa kuhakikisha anakuwa mfano wa wachezaji watakaotimiza ndoto za kufika mbali.
    Kivipi? Dogo dizaini ametosheka fulani hivi na maisha ya Lubumbashi- lakini hapana. Anatakiwa kufunguka zaidi na kutafuta nafasi ya kucheza Ulaya ndani ya miaka hii miwili ajiwekee malengo ya kuhakikisha amekwishatoka Afrika.
    Hawezi kutoka kwa maneno, atufungie mabao pale Taifa Stars kwa juhudi zake binafsi watu wakiri kijana ni hatari kwa uwezo wa soka yake uwanjani na si minyoo ya kisasa na mitindo ya mavazi nje ya uwanja.
    Samatta anacheza hapo tu DRC, lakini Nizar alikuwa Marekani na amecheza Ligi Kubwa zaidi dhidi ya wachezaji wakubwa zaidi- leo amerudi nyumbani kusaini Yanga. Mimi sitapenda kuona Samatta naye akirejea nyumbani karibuni, nataka afike mbali. Alamsiki!
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA HAPO TU DRC, NIZAR ALIKUWA ANAKIPIGA MAREKANI! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top