• HABARI MPYA

    Thursday, October 04, 2012

    BOBAN ALIVYOISAIDIA YANGA JANA…

    Boban akihojiwa na Waandishiwa Habari

    Na Mahmoud Zubeiry 
    KIUNGO Haruna Moshi Shaaban ‘Boban’ alitokea benchi na moja kwa moja kwenda kumuumiza beki kizingiti wa Yanga, Kevin Yondan hadi akashindwa kuendelea na mchezo wa wapinzani wa jadi, jana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Kweli Yanga ilipata pigo kumpoteza beki wake mahiri, Yondan, lakini kwa mabadiliko yaliyofanywa na kocha Mholanzi, Ernie Brandts timu hiyo iliimarika zaidi.
    Beki huyo wa zamani wa kimataifa wa Uholanzi, aliyeng’ara kwenye Fainali za Kombe la Dunia mwaka 1978, alimuingiza Juma Abdul badala ya Yondan.
    Abdul akaenda kucheza beki ya kulia alikokuwa anacheza Mbuyu Twite, ambaye alihamia katikati kuziba pengo la Yondan.
    Kutoka hapo Yanga, ilianza kucheza vizuri kila idara ikionyesha mchango wake uwanjani. Kwa nini? Yanga wamekuwa wakilazimisha kumpanga Mbuyu, wakati huo huo inataka kutumia mabeki wengine wa kati ilionao, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Yondan.  
    Haikuwa vibaya Yanga kumsajili Mbuyu Twite, kwa sababu baada ya Cannavaro na Yondan, beki mwingine wa kati waliyekuwa naye ni Ibrahim Job pekee.
    Niliamini kusajiliwa kwa Twite, maana yake Yanga itakuwa na mabeki wawili wa kati uwanjani na wawili benchi, lakini sasa si hivyo.
    Ni kama Yanga imeridhika na uchezaji wa pamoja wa Yondan na Cannavaro, lakini inalazimisha na Twite acheze.
    Mwanzoni, Twite alikuwa anapangwa kama kiungo mkabaji, lakini akashindwa kucheza kwa ubora wa Athumani Iddi ‘Chuji’, hivyo akahamishiwa beki ya pembeni.
    Morogoro dhidi ya Mtibwa alipangwa beki ya kushoto, akawa uchochoro wa Hussein Javu na mechi nyingine zilizofuata amekuwa akicheza beki ya kulia- pia uchezaji wake hauridhishi kama ambavyo wanacheza Juma Abdul, Godfrey Tauta, au Nahodha Nsajigwa Shadrack wenye nafasi yao.
    Jana hilo limedhihirika, wakati anacheza beki ya kulia, Twite pamoja na kusaidia sana mashambulizi, lakini alikuwa anashindwa kumdhibiti Edward Christopher, ila alipoingia Juma Abdul alitekeleza jukumu hilo vema, akizuia na kusaidia mashambulizi.
    Hata Twite alipohamia katikati, alicheza vizuri na ubora wake ule uliofanya agombewe na Simba na Yanga ulionekana.
    Twite ni beki wa kati na naamini anaweza kucheza vizuri nafasi hiyo tu, hizo nyingine analazimishwa kwa sababu ni mchezaji nyota na wenye timu yao hawataki aanzie benchi.
    Lakini wapo watu waliosajiliwa maalum kwa ajili ya nafasi hizo, tena wengi mno. Katika nafasi ambazo Yanga imewekeza vizuri kwenye timu yake, basi ni mabeki wa pembeni.
    Kulia peke yake wapo watatu, Nsajigwa, Abdul na Taita na kushoto pia wapo watatu, David Luhende, Oscar Joshua na Stefano Mwasyika, sasa kama beki wa kati anapelekwa pembeni, hawa waliosajiliwa kwa ajili ya kucheza nafasi hizo wacheze wapi?
    Hapa sasa unaweza kuona Twite anaivuruga Yanga kwa kulazimishwa kucheza na kitu kingine ambacho sielewi Yanga ni kuwachezesha mbele mabeki wa pembeni, wakati timu ina viungo wengi tu wa pembeni.
    Mara nyingi makocha wengi duniani hutumia mabeki mbele katika kujihami na sana hutokea katika mechi ngumu, kama fainali kocha anajua anakutana na timu yenye kushambulia sana, hivyo anaongeza wakabaji uwanjani.
    Kweli Boban alipomuumiza Yondan, aliiathiri Yanga, lakini upande wa pili aliisaidia sana. Kwa sababu asingemtoa uwanjani Yondan, ina maana Twite angeendelea kuwa uchochoro kule kulia na lolote lingetokea.
    Ila kwa sababu Yondan alitoka, yakafanyika mabadiliko yaliyoisaidia Yanga.  
    Mbuyu Twite

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BOBAN ALIVYOISAIDIA YANGA JANA… Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top