• HABARI MPYA

    Tuesday, October 02, 2012

    SIMBA WAMGUNA REFA AKRAMA, WAKATA TAMAA NA SEKRETARIETI TFF

    Ofisa Habari wa Simba SC, Ezekiel Kamwaga akizungumza na Waandishi wa Habari makao makuu ya klabu, Mtaa wa Msimbazi, Dar es Salaam leo kuhusu Akrama.

    Na Mahmoud Zubeiry
    KLABU ya Simba SC imeshangazwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kumpanga refa Mathew Akrama wa Mwanza kuchezesha mechi mbili mfululizo za Yanga katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Ofisa Habari wa Simba SC, Ezekiel Kamwaga amesema asubuhi ya leo katika Mkutano na Waandishi wa Habari makao makuu ya klabu,Mtaa wa Msimbazi, Dar es Salaam kwamba Akrama atakayechezesha pambano la watani wa jadi kesho, ndiye aliyechezesha mechi iliyopita ya Yanga na African Lyon.
    “Kwa nyinyi ambao hamna taarifa labda, lakini sisi tulikuwa tuna taarifa kwamba, kuna refa mwingine alipangwa kuchezesha mechi ya Yanga na African Lyon, lakini akabadilishwa akawekwa Akrama,”alisema Kamgwa.
    Aidha, Kamwaga aliitupia lawama Sekretarieti ya TFF kwa kutowatendea haki kwenye mambo mengi, likiwemo suala la usajili wa mabeki Kevin Yondan na Mbuyu Twite.
    “Tunajua sekretarieti ya TFF ndiyo huwa inahusika kupanga marefa, na ndiyo hii hii ambayo tunailalamikia haitutendei haki, sasa sisi tunamuomba mambo mawili makubwa Akrama, kwenye mechi ya Simba na Yanga; kuna watu huwa wanapoteza maisha wakifungwa. Kuna watu huwa wanapoteza fahamu, wanaweka rehani nyumba zao, mali zao kucheza kamari, na wanaliwa.kuna viongozi wengine wamewahi kutimuliwa madarakani kwa sababu ya kufungwa na Simba na Yanga.
    Kwa hiyo, hii mechi ina mambo mengi sana, sasa sisi tunamuomba Akrama asiue watu, asifanye watu wakaliwa, asifanye watu wakapata mateso yasiyo na sababu,”alisema.
    Kamwaga alisema Simba haitaki kutetewa na refa huyo na haitarajii upendeleo wowote kutoka wake na wala haitaki upendeleo wowote kutoka kwa Akrama. “Ila tunachomuomba, atende haki. Achezeshe kwa kufuata sheria 17 za soka,”alisema.
    Kamwaga aliongeza kuwa, kwa sababu hiyo itaonyeshwa na Televisheni ya Super Sport, ni vema Akrama akaitumia fursa hiyo kujipromoti katika medani ya kimataifa ya soka kama refa bora.
    “Mwaka jana katika Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, Tanzania haikuwa na refa wala mshika kibendera hata mmoja, kwenye Kombe la Dunia, ndiyo usiseme. Sasa inatia aibu kwa kweli kwa nchi kubwa kama Tanania, ambayo ina historia kubwa lakini haina marefa kwenye mashindano makubwa, Akrama kama atachezesaha vizuri kesho, itamjenga na anaweza kubebwa kwenye mashindano makubwa ya FIFA na CAF,”alisema Kamwaga.
    Ofisa Habari huyo wa Simba, alilalamikia pia klabu yake kutopewa barua ya kudai fedha za Twite, kama ambavyo Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) iliagiza.
    “Tumepata barua ya Okwi kufungiwa mechi tatu bila kuomba, lakini hadi leo, hatujapata barua ya kudai fedha za Twite, tulituma barua ya kuomba kukazia maamuzi ya sheria. Hadi jana tunauliza maamuzi ya Kamati kwa maandishi, lakini hadi sasa hayajaandikwa.
    Basi watuandikie barua ya kukata fedha zetu kwenye mechi ya kesho. Hiyo pia inawashinda kuandika. Mmoja wa viongozi wa TFF, alituambia tuwaandikie barua Yanga, kuomba tukate fedha zao. Tunaona hiyo siyo sahihi, tunaona Sekretarieti ya TFF haina dhamira ya kututendea haki, maana yake siku 21 zilizotolewa kama muda wa sisi kulipwa fedha zetu za Twite, zinaisha kesho na hakuna dalili za kupata hizo fedha,”alisema Kamwaga.
    Septemba 10, mwaka huu Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji, chini ya Mwenyekiti wake, Alex Mgongolwa ilitoa maamuzi ambayo hayakuwaridhisha walalamikaji, Simba SC juu ya Twite na Yondan na sasa wanataka kulipeleka suala hilo CAS.
    Kamati hiyo, iliitaka Simba kuthibitisha madai yake ya kuingia mkataba na Yondan na kuwasilisha upya malalamiko yake kwenye kamati hiyo.
    “Kwa mujibu wa Ibara ya 44 (3) ya Kanuni za Uhamisho wa Wachezaji za TFF, Yanga ilifuata taratibu zote katika kumsajili Kevin Yondan, hivyo ni mchezaji wake halali.
    Kwa vile Simba imesema mchezaji huyo vilevile alisaini mkataba na klabu yao, imetakiwa kupitia mamlaka nyingine kuthibitisha hilo, na baada ya uthibitisho iwasilishe malalamiko yake kwenye Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji, au mamlaka zozote za kisheria kwa mujibu wa madai/lalamiko husika,”alisema Mgongolwa.
    Kuhusu suala la Mbuyu Twite, Mgongolwa alisema kwamba kwa mujibu wa Ibara ya 18(3) ya Kanuni za Hadhi na Uhamisho wa Wachezaji wa Kimataifa za FIFA, Yanga ilifuata taratibu zote katika kumsajili Mbuyu Twite, hivyo ni mchezaji wake halali.
    Hata hivyo, alisema kwa vile Yanga imekiri kuwa mchezaji huyo alichukua dola 32,000 za Simba na kukiri kuzirejesha,kwa msingi wa kanuni ya Fair Play, Kamati imeipa Yanga siku 21 iwe imelipa fedha hizo Simba.
    Wajumbe sita kati ya saba waliopo walihudhuria kikao hicho chini ya Mwenyekiti Alex Mgongolwa. Wajumbe hao ni Hussein Mwamba, Imani Madega, Ismail Aden Rage, Llyod Nchunga na Omari Gumbo.
    Siku 21 walizopewa Yanga kurudisha fedha za Twite alizochukua Simba, zinamalizika kesho, siku ambayo watani hao wa jadi katika soka ya Tanzania, watamenyana katika mchezo wa Ligi Kuu, mzunguko wa kwanza.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA WAMGUNA REFA AKRAMA, WAKATA TAMAA NA SEKRETARIETI TFF Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top