• HABARI MPYA

    Tuesday, October 16, 2012

    AZAM FC KUIONJA SOKOINE LEO

    Azam FC

    Na Mahmoud Zubeiry
    AZAM FC leo jioni watafanya mazoezi kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, ili kuuzoea kabla ya mechi ya kesho dhidi ya wenyeji, Prisons katika mfululizo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Mabingwa hao wa Kombe la Mapinduzi na washindi wa pili wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame wapo mjini Mbeya tangu juzi saa 1:00 usiku na jana walifanya mazoezi kwenye Uwanja wa sekondari ya Iyunga mjini humo.
    Kikosi kizima cha Azam kipo vizuri kuelekea mchezo unaitarajiwa kuwa mgumu kwao na wachezaji wa morali ya ushindi, ili kuweka vizuri mazingira ya kutwaa taji la kwanza la ubingwa wa Ligi Kuu ya Bara.
    Azam waliondoka Morogoro juzi asubuhi baada ya mechi yao na Polisi kwenye Uwanja, Jamhuri Jumamosi ambayo walishinda 1-0, bao pekee la mshambuliaji kutoka Ivory Coast, Kipre Herman Tchetche.
    Mbeya ni kati ya vituo ambavyo vinawaogopesha vigogo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Azam, Simba na Yanga kutokana na imani kwamba Prisons haifungiki kwenye Uwanja wake.
    Sababu kubwa ni ubovu wa Uwanja wa Sokoine, ambao wenyewe Prisons wameuzoea na wanaujulia, wakati timu nyingine hupata tabu mno.
    Kati ya vigogo hao watatu, ambao wanafukuzana kuwania ubingwa wa Ligi Kuu, Azam inakuwa timu ya pili kwenda Mbeya, baada ya Yanga iliyolazimishwa sare ya bila kufungana na Wajelajela hao kwenye mechi yao ya kwanza ya ligi hiyo.
    Simba imeanzia Dar es Salaam kucheza na Prisons, Septemba 29, mwaka huu katika mechi ambayo walishinda kwa taabu mabao 2-1 na sasa watarudiana na Wajelajela hao mjini Mbeya katika mzunguko wa pili wa ligi hiyo.   
    Mikoa mingine tishio ni Kanda ya Ziwa, ambako Azam tayari imekwishamaliza na kukusanya pointi nne baa ya kuifunga 1-0 Kagera Sugar Uwanja wa Kaitaba kabla ya kulazimishwa sare ya 2-2 na Toto Africans Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.
    Yanga pia imemaliza deni la Kanda ya Ziwa, ikiambulia pointi tatu, baada ya kufungwa 1-0 na Kagera na kushinda 3-1 dhidi ya Toto. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: AZAM FC KUIONJA SOKOINE LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top