Oden Mbaga kulia akimuonya Haruna Moshi 'Boban' wakati wa mechi kati ya Taifa Stars na Malawi, Mei 26, mwaka huu. Kulia ni kiungo wa The Flames, James Sangala aliyechezewa rafu na Haruna. |
Na Prince Akbar
REFA Oden Mbaga wa Tanzania anayetambuliwa na Shirikisho la Soka
la Kimataifa (FIFA) ndiye anayechezesha mechi ya kirafiki kati ya Kenya
(Harambee Stars) na Afrika Kusini (Bafana Bafana).
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface
Wambura ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba mechi hiyo inachezwa leo Uwanja wa
Kimataifa wa Moi Kasarani jijini Nairobi na Mbaga atasaidiwa na marefa
wasaidizi wa FIFA, John Kanyenye kutoka Mbeya na Erasmo Jesse wa Morogoro.
Amesema TFF imeteua marefa hao baada ya kupata maombi kutoka
kwa Shirikisho la Soka Kenya (FKF) ambao ndiyo waandaaji wa mechi hiyo ambayo
ni moja ya vipimo kwa kocha mpya wa Harambee Stars, Henry Michel kutoka
Ufaransa.
Wakati huo huo: Wambura Kamati ya Uchaguzi ya Chama cha
Makocha wa Soka Tanzania (TAFCA) imeongeza muda kwa wagombea kuchukua fomu kwa
ajili ya uchaguzi wa chama hicho ambao sasa utafanyika Novemba 25 mwaka huu.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TAFCA,
Ramadhan Mambosasa, jana ndiyo ilikuwa mwisho wa kuchukua fomu lakini mwitikio
wa wagombea bado umekuwa mdogo ambapo ni watano tu waliojitokeza.
Hivyo, amesema wameongeza muda wa kuchukua na kurudisha fomu
ambapo mwisho itakuwa ni Oktoba 19 mwaka huu saa 10 kamili alasiri. Fomu
zinapatikana ofisi za TAFCA ambazo ziko Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es
Salaam.
Nafasi zinazogombewa ni Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu
Mkuu, Katibu Msaidizi, Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF, Mhazini na wajumbe watatu
wa Kamati ya Utendaji.