Ngassa |
Na Mahmoud Zubeiry
MRISHO
Khalfan Ngassa ameanza mazoeizi jana timu yake Simba SC kwenye Uwanja wa Kinesi, Urafiki, Dar es Salaam, lakini amesema bado
hayuko sawa sawa, maana yake uwezekano wa kucheza mechi ya kesho dhidi ya timu
yake ya zamani, Kagera Sugar Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ni mdogo.
Akizungumza
na BIN
ZUBEIRY jana, Ngassa ambaye aliugua Malaria baada ya mechi dhidi ya
Yanga, Oktoba 3, mwaka huu alisema kwamba bado anahisi hana nguvu.
“Nimeanza
mazoezi na timu, lakini hata hivyo bado hali yangu haiko sawa sawa kwa kweli,
najisikia mwili hauna nguvu, hii Malaria ilinipelekesha sana, ila najikongoza
hivyo hivyo,”alisema Ngassa.
Kiungo
mwingine wa Simba SC aliyekuwa anaumwa Malaria, Ramadhani Chombo ‘Redondo’ naye
ameanza mazoezi na timu na anaweza kucheza kesho.
Mbali na
Redondo, katika mchezo huo, Simba inatarajiwa kuwapokea wachezaji wake wengine watatu
iliyowakosa kwenye mechi iliyopita dhidi ya Coastal Union Jumamosi Uwanja wa
Mkwakwani, Tanga ambayo iliisha kwa sare ya bila kufungana, Emmanuel Okwi
aliyekuwa kwao Uganda kuichezea timu yake ya taifa, Komabil Keita, Haruna
Shamte na Kiggi Makasy waliokuwa majeruhi.
Mechi
nyingine za kesho zitakuwa kati ya Prisons na Azam FC kwenye Uwanja wa Sokoine,
Mbeya, Polisi Morogoro na JKT Ruvu Uwanja wa Jamhuri, Morogoro, Mgambo JKT na
Toto Africans Uwanja wa Mkwakwani, Tanga na JKT Oljoro dhidi ya African Lyon
Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha.
Simba bado
ipo kileleni mwa Ligi Kuu kwa pointi zake 17, baada ya kucheza mechi saba,
ikifuatiwa na Azam FC yenye pointi 16, ambayo hata hivyo imecheza mechi sita,
wakati Yanga inashika nafasi ya tatu kwa pointi zake 11, baada ya kucheza mechi
saba pia.