Wachezaji wa Yanga wakipasha |
Na Mahmoud Zubeiry
KIKOSI cha Yanga
kinatarajiwa kuingia kambini leo katika hoteli ya Uppland, Changanyikeni, Dar
es Salaam kujiandaa na mchezo wao ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara
dhidi ya Ruvu Shooting Jumamosi wiki hii kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Yanga
ilikwama kuingia kambini jana ilivyopanga na badala yake sasa wataingia leo
Changanyikeni, ili kuziweka fikra za wachezaji pamoja kuelekea mechi hiyo ya
Jumamosi.
Habari njema ni kwamba, beki Kevin Yondan jana alianza
mazoezi mepesi kwenye Uwanja wa sekondari ya Loyola, Dar es Salaam, ikiwa ni
mara ya kwanza tangu agongwe na kiungo wa Simba, Haruna Moshi ‘Boban’ katika
mechi baina ya wapinzani hao wa jadi, Oktoba 3, mwaka huu.
Pamoja na Yondan, mshambuliaji Said Bahanuzi aliyekuwa
anasumbuliwa na maumivu ya nyama za paja naye alianza pia mazoezi mepesi jana kwenye
Uwanja wa sekondari ya Loyola, Dar es Salaam.
Bahanuzi
‘Spider Man’ alichanika nyama za paja la mguu wa kulia katika mechi ya Ligi Kuu
ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba
Jumatatu wiki iliyopita.
Bahanuzi aliumia
dakika ya 23, baada ya kugongana na beki Benjamin Effe wa Kagera Sugar na
kushindwa kuendelea na mchezo, nafasi yake ikichukuliwa na Jerry Tegete katika
mechi ambayo Yanga ililala 1-0, beo pekee la Themi Felix.
Bahanuzi
ndiye tegemeo la mabao la Yanga kwa sasa, kwani tangu ajiunge na timu hiyo
akitokea Mtibwa Sugar msimu huu, ameifungia mabao 12 katika mechi 13, ikiwemo
ile dhidi ya Kagera aliyocheza kwa dakika 23 kabla ya kuumia na kutoka.
Yanga kwa
sasa inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu kwa pointi zake 11,
baada ya kucheza saba, kushinda tatu, sare mbili na kufungwa mbili.
Simba
iliyocheza mechi saba pia, inaongoza ligi hiyo kwa pointi zake 17, ikifuatiwa
na Azam FC yenye pointi 16, iliyocheza mechi sita.