![]() |
Na Mahmoud Zubeiry |
KATIKA Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF)
mwaka huu- jambo ambalo naweza kuliita kubwa lilikuwa ni kuteuliwa kwa Said
Hamad El Maamry na Muhiddin Ahmad Ndolanga kuwa marais wa heshima wa shirikisho
hilo.
Wawili hawa, wote ni viongozi wa zamani wa juu wa soka ya
Tanzania, ambao viongozi waliowafuatia wameshindwa kuvunja rekodi zao hadi
sasa.
El Maamry, wakati wake soka ilikuwa ina heshima, hadhi na
mafanikio na ni wakati wake ndipo Tanzania ilicheza Fainali za Kombe la Mataifa
ya Afrika mwaka 1980 nchini Nigeria.
Jambo moja tu, ambalo wachezaji wa zamani wamekuwa ‘wakimlaani’
El Maamry alibana mno wachezaji wa Tanzania kucheza nje na pia katika hilo
inawezekana walikuwa wanamuonea, pengine ilitokana na sera za nchi wakati huo,
ambazo yeye labda alishindwa kupambana nazo.
Ndolanga, alikuwa ana wakati mgumu sana katika utawala wake,
pamoja na kwamba alijitahidi kupambana na chuki na vita dhidi yake na wakati
huo huo alifanya jitihada za kupanga mikakati na kutekeleza mipango ya
maendeleo ya soka ya Tanzania.
Alhaj Ndolanga wakati wake walimuita Tyson, eti wakimuona ni
mbabe kutokana na misimamo yake- lakini leo ukitazama hali halisi enzi zake,
unagundua babu alitolewa ‘kafara’ tu.
Mambo yasiyopungua matatu yalimkwamisha Ndolanga katika
utawala wake, katiba mbovu iliyotoa fursa ya migogoro na mapinduzi, pili timu
au watu aliokuwa akifanya nao kazi kuwa aidha wasaliti au watu wenye upeo mdogo
na wasio waadilifu na tatu ni Profesa Juma Athumani Kapuya, ambaye alikuwa
anamuingilia mno na kuonekana dhahiri anampiga vita wakati akiwa Waziri
anayehusika na michezo.
Madudu mangapi yalifanywa na Kapuya akiwa Wizara ya michezo
tena ya kihistoria, lakini nitakumbushia machache tu. Kuingilia mfumo wa Ligi
Kuu kwa kuongeza timu kinyume na makubaliano kati ya FAT na waliokuwa
wadhamini, Bia ya Safari Lager hadi wakaamua kujitoa mwaka 2001 na kusababisha
timu zikose fedha za udhamini, ikiwemo zawadi za washindi mbalimbali hadi
bingwa wa mwaka huo, Simba SC.
Kuingilia na kuvuruga usajili, kuamua bingwa mezani mwaka
1999, wakati Yanga tayari imetwaa taji kwa matokeo ya uwanjani, akapitia rufaa
na kutoka matokeo, akawapa ubingwa Mtibwa Sugar. Jamani ni mengi na
hatujasahau, kwani kiasi kikubwa miaka 10 ya Kapuya kuwa kwenye wizara yenye
dhamana ya michezo, ilikuwa kikwazo kikubwa cha maendeleo ya mchezo huu na
mingine mingi nchini.
Alishindwa kuondoka amri ya kuzuia michezo mashuleni, akiwa
Waziri mwenye dhamana ya michezo- hakujua kama wanamichezo wazuri huanzia
kutengenezwa wangali wadogo mashuleni. Aliona poa tu. Kapuya huyo! Profesa.
Pamoja na yote, Ndolanga alionyesha uhodari wake kwa
kuendelea kuongoza soka ya nchi hii licha ya hali ngumu pia ya kiuchumi wakati
huo, kutokana na wadau, makampuni kutosaidia mchezo huo, kwa kuamini umegubikwa
na fujo na migogoro.
Timu ya taifa haikuwa na wadhamini, alijaribu kuwahusisha
wafanyabiashara wakubwa kama Reginald Mengi, Azim Dewji, Mohamed Dewji na
wengineo kusaidia timu. Tulishiriki mashindano karibu yote, kuanzia ya vijana,
wanawake na wakubwa.
Msisimko wa soka ya Tanzania enzi za utawala wa Ndolanga ni
tofauti mno na ligi laini laini tunayoiona leo. Kama yapo mabaya ya Ndolanga
aliyeanza kuongoza soka ya nchi hii mwaka 1991 katika kamati ya Muda, kabla ya
kuchaguliwa rasmi 1993 kwa kura na kudumu hadi 2004, alipoangushwa na Leodegar
Chilla Tenga, hakuna hakika kwenye mizani yatazidi mazuri yake.
Fursa ambayo ameipata Tenga ya kuungwa mkono na wadau,
makampuni, wafadhili, serikali na kulindwa na katiba mpya iliyotokana na mwongozo
wa FIFA, Uwanja mpya wa Taifa hapana shaka na Ndolanga angevipata, leo
tungekuwa tunazungumza lugha tofauti kuhusu yeye.
Si wakati wa kuoneana haya tena, zaidi ya kuambiana ukweli
kwa manufaa ya soka yetu. Sijali, atakayenichukia, kunitenga shauri yake,
lakini daima nitasimamia katika ukweli na hiyo kwa sababu ya uzalendo wangu na
mapenzi yangu katika soka. Miaka nane ya Tenga kuwapo madarakani, imetosha
kujua uwezo wake na kwa kumlinganisha na Ndolanga, jibu lipo wazi. Kipindi
kigumu alichopitia Ndolanga, na hali halisi ya soka yetu ilivyokuwa kama
nilivyoelezea hapo juu, kulinganisha na mambo yalivyo sasa, inamaanisha babu
alikuwa ‘babu kubwa’.
Tanzania aliyoiongoza Mwalimu Julius Kabarage Nyerere, si
Tanzania anayoiongoza Jakaya Mrisho Kikwete leo. Tanzania ya leo ni nzuri na
changamoto kubwa inayowakabili wakuu wa nchi ni kupanuka kwa demokrasia na
uhuru wa maoni, lakini nchi ile aliyoiongoza Mwalimu, hakuna hakika kama
Jakaya, Benjamin William Mkapa au Ally Hassan Mwinyi wangeiweza. Vivyo hivyo, mazingira
aliyofanyia kazi Ndolanga katika soka ya nchi hii, dhahiri Tenga asingeweza.
Tena kabisa.
Pamoja na mengi ambayo tunaamini yalikuwa mazuri kutoka kwa
Ndolanga, kubwa lililokuwa linavutia wengi ni jinsi alivyowathamini makocha
wazawa, kuwapa fursa za kujiendeleza kielimu na kuwapa majukumu ya kufanya kazi
katika timu za taifa.
Tangu mwaka 1991 hadi 2004, Ndolanga ameacha hazina kubwa ya
makocha wazawa wa kiwango cha kimataifa ambao ndio leo TFF ya Tenga inawatumia
kama ‘madeiwaka’ akina Charles Boniface Mkwasa na Sylvester Marsh. Labda watu
watakuwa hawajui kuhusu Marsh, huyu jamaa alikuwa anafundisha watoto Mwanza,
Ndolanga alimuona huko akamchukua na kumuendeleza kabla ya kumpa majukumu ya
kufundisha timu za taifa za vijana.
Hata lilipokuja shinikizo la kuleta kocha wa kigeni, bado
imani ya Ndolanga ilibaki kwa makocha wazawa- kwa mfano mwaka 2002 kulikuwa
kuna kocha Mjerumani Burkhad Pape, ila baada ya miaka miwili ya kuwapo kwake
nchini kama kocha mkuu wa timu ya taifa bila mafaniko yoyote, akaamua kumfanya
Mkurugenzi wa Ufundi na Syllersaid Salmin Kahema Mziray (sasa marehemu) pamoja
na Charles Boniface Mkwasa wakapewa jukumu la ukocha wa timu ya taifa.
Kwa mabadiliko hayo, Tanzania ikatwaa Kombe la kwanza lenye
hadhi ya Afrika, CECAFA Castle Cup, mwaka 2002 michuano iliyokuwa
inashirikisha timu za taifa za Afrika
Kusini, DRC, Ghana na jirini zetu Kenya na Uganda. Mwaka huo huo, Tanzania
ikafika fainali ya Kombe la Challenge kwa mara ya kwanza baada ya miaka sita na
kufungwa na Kenya 3-2 na Kenya mjini Mwanza.
Kenya iliyoifunga Tanzania ilikuwa ina kikosi kikali haswa,
ambacho miaka miwili baadaye ilifuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya
Afrika nchini Tunisia, kikiundwa na wakali kama Mussa Otieno, Dennis Oliech,
John Oliech, Titus Mulama, Geoffrey Mangenge ‘Osama’ na wengineo.
Tulizikosa kosa kidogo tu fainali za Kombe la Mataifa ya
Afrika 1996 nchini Burkina Faso, kama si kufungwa mechi ya mwisho na Algeria
Julai 30, mwaka 1995 mjini Algiers mabao 2-1, siku hiyo Nahodha wetu Stars enzi
hizo, Hussein Amaan Marsha akiwafungia bao la kusawazisha wapinzani dakika ya
29, baada ya Mohamed Hussein Daima ‘Mmachinga’ kuifungia Tanzania bao la
kuongoza dakika ya 21, kabla ya Amrouche kutupiga bao la pili dakika ya 59 na
kuipa Algeria tiketi ya kwenda Burkina Faso, ikiungana na vinara wa kundi letu,
Misri.
Misri ilimaliza na pointi 15, Algeria waliokuwa wa pili
pointi 13, Uganda waliokuwa wa tatu walimaliza na pointi 10, wakati sisi
(Tanzania) katika nafasi ya nne tulimaliza na pointi nane. Ila kama
tungewafunga Algeria, wangebaki na pointi zao 10, hivyo tungefikisha pointi 11
na kuwa wa pili na kufuzu kwenye fainali hizo.
Pamoja na kwamba kwenye kampeni hizi kocha Mbrazil Clovis de
Oliviera alihusika, lakini bado kulikuwa kuna mchango mkubwa wa makocha
wazalendo akina Mzee Heri na Kayuni. Hakika kwa hili makocha wazawa
watamkumbuka sana Ndolanga, ambaye kwa sasa yupo nje ya ulingo wa soka, baada
ya kuangushwa kwenye uchaguzi mwaka 2004. Na kwa sababu hiyo, leo nawapongeza
TFF, hawakukosea kuwapa heshima hiyo El Maamry na Ndolanga.
0 comments:
Post a Comment