RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan ameipongeza Simba SC kwa ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Stellenbosch FC ya Afrika Kusini katika mchezo wa kwanza was Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika jioni ya leo Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.
“Hongera sana kwa Klabu ya Simba kwa ushindi katika mchezo wa Mashindano ya Kombe la Shirikisho la Soka Afrika (CAF Confederation Cup). Mmeleta furaha kwa mashabiki wenu na Watanzania wote na kuipeperusha vyema bendera ya nchi yetu,”:
“Motisha kutoka kwangu mtaipokea kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. Ninawatakia kila la kheri,” amesema Mheshimiwa Rais katika taarifa yake jioni ya leo.
Kwa upande wake Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraka la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amewapongeza wachezaji wa timu ya Simba kwa ushindi walioupata katika mashindano ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika, katika mchezo wa awali wa Nusu Fainali dhidi ya timu ya Stellenbosch Football Club ya Afrika Kusini.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi ametoa pongezi hizo akiwa katika makaazi yake ya Ikulu Ndogo Migombani, Zanzibar, akifuatilia mchezo huo uliochezwa katika Uwanja wa New Amaan Complex, Wilaya ya Mjini, Mkoa wa Mjini Magharibi tarehe 20 Aprili 2025.
Halikadhalika, Rais Dkt.Mwinyi ameipongeza timu ya Simba kwa kuuchagua Uwanja wa New Amaan Complex kuwa uwanja wao wa nyumbani na kueleza kuwa Serikali imefarijika na hatua hiyo, huku akiahidi kuendelea kuimarisha viwanja mbalimbali hapa Zanzibar.
Pongezi kwa mfungaji wa bao hilo pekee, kiungo wa Kimataifa wa Ivory Coast, Jean Charles Ahoua dakika ya 45'+2 kwa shuti la kitaalam la mpira wa adhabu lililomshinda kipa wa Afrika Kusini, Oscarine Masuluke.
Baada ya mchezo huo, Naibu Waziri wa Uatamaduni, Sanaa na Michezo, Hamisi Mwinjuma ‘Mwana FA’ aliwakabidhi Simba SC zawadi ya Sh. Milioni 20 kutoka kwenye Mfuko wa Rais Samia, maarufu kama ‘Goli la Mama’ kutokana na ahadi ya kupatiwa Sh. Milioni 20 kwa kila watakalofunga.
0 comments:
Post a Comment