JKU YAITUPA NJE SINGIDA BLACK STARS KOMBE LA MUUNGANO
TIMU ya JKU imefanikiwa kutinga Nusu Fainali ya Kombe la Muungano baada ya ushindi wa penalti 6-5 dhidi ya Singida Black Stars jioni ya leo Uwanja wa Gombani, Pemba.
Katika dakika 90 za kawaida za mchezo mabao ya JKU yamefungwa na Tariq Mohamed dakika ya 28 kwa penalti na Freddy Suleiman dakika ya 45’+3, wakati ya Singida Black Stars yamefungwa na Victorien Adebayor dakika ya sita na Iddi Khalid dakika ya 25.
Michuano hiyo maalum ya kuazimisha sherehe za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliozaa Tanzania tukufu Aprili 26, mwaka 1964 itaendelea kesho kwa Zimamoto kuumana na Coastal Union ya Tanga Aprili 25 kuanzia Saa 10:00 jioni, kabla yan KMKM watacheza Azam FC ya Dar es Salaam kuanzia Saa 1:15 usiku hapo hapo Uwanja wa Gombani.
Vigogo, Yanga watakamilisha hatua hiyo ya Robo Fainali kwa kumenyana na wenyeji wengine, KVZ Jumamosi kuanzia Saa 1:15 usiku — wakati mechi za Nusu Fainali zitafuatia Aprili Jumatatu na Jumanne na Fainali itachezwa Mei 1 hapo hapo Uwanja wa Gombani.
Mabingwa watetezi, Simba wameshindwa kushiriki michuano ya mwaka huu kwa sababu wanakabiliwa na mechi ya marudiano ya Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Stellenbosch ya Afrika Kusini Aprili Jumapili Jijini Durban.
Simba SC ilitwaa taji la michuano hiyo iliyoanza mwaka jana kwa ushindi wa 1-0 dhidi ya Azam FC katika Fainali Uwanja wa New Amaan Complex, bao pekee la kiungo Msenegal, Babacar Sarr, dakika ya 77.
Sarr alifunga bao hilo akimalizia mpira wa adhabu uliopigwa na beki Israel Patrick Mwenda kufuatia mshambuliaji Mcameroon, Leandre Willy Essomba Onana kuangushwa nje kidogo ya boksi.
Simba SC ilizawadiwa Sh. Milioni 50, wakati washindi wa pili, Azam FC walipata Sh. Milioni 30.
0 comments:
Post a Comment